Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa amemkaribisha aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu, ambaye amejivua nyadhifa zote alizokuwa nazo CCM. Akionyesha kuwa na furaha leo Jumatatu wakati akiongea, Lowassa hakuwa na maneno mengi, akiyafupisha kwa kusema “tumelamba dume”. Nyalandu (47), ambaye pia alikuwa mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, alitumia nafasi hiyo kuomba kujiunga na Chadema, akisema anaiomba imfungulie mlango. Dakika chache tangu Nyalandu aombe kujiunga na Chadema, Lowassa alimkaribisha waziri huyo wa zamani wa Maliasili na Utalii huku akisema mwanasiasa huyo amechelewa kujiunga na upinzani. “Mbona amechelewa? Alitakiwa awe amejiunga muda mrefu, tena hasa wakati wa Uchaguzi Mkuu. Ninamkaribisha sana kwa sababu ni mwanasiasa mzuri na anayejua majukumu yake,” alisema Lowassa ambaye alikuwa waziri mkuu wa kwanza katika Serikali ya Awamu ya Nne. “Nyalandu ni hazina, ni mbunge imara na ni mwanasiasa wa mfano,” alisema Lowa...